PODCAST · news
Habari za UN - Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu
by United Nations
Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu
-
100
06 JULAI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina. Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendelo, UNDP, nchini Tanzania kupitia mradi wake wa Dumisha Amani awamu ya pili, unaotekelezwa kwa kushirikiana na serikali ya nchi hiyo limeendesha midahalo ya amani na utatuzi wa migogoro kwa vijana, lengo, ni kuimarisha amani kwa Maendeleo Endelevu.Siku nne tu baada ya shambulio kubwa la Urusi dhidi ya Ukraine, usiku wa kuamkia leo kwa saa za Ukraine wakazi wa Mji Mkuu, Kyiv kwa mara nyingine tena wamekumbana mashambulizi yaliyofanywa na Vikosi vya Wanajeshi wa Urusi. Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa nchini humo, Matthias Schmale, amesisitiza akisema, "haiwezi kurudiwa mara nyingi vya kutosha kwamba sheria za kimataifa za kibinadamu zinataka hatua zote zinazowezekana zichukuliwe ili kuwalinda raia na miundombinu ya kiraia." Mbali na mji mkuu, mwishoni mwa wiki mashambulizi ya mabomu katika mji wa Sumy yaliwaua raia kadhaa na kuwajeruhi makumi ya wengine, wakiwemo watoto. Miji mingine kama Dnipro, Kherson, Kyiv, Zaporizhzhia na mingine pia ilikumbwa na vifo na majeruhi wengi miongoni mwa raia pamoja na uharibifu mkubwa wa miundombinu ya kiraia, hali iliyokatiza upatikanaji wa huduma za msingiHakuna dawa au mwanasesere anayefikia mtoto bila kufanyiwa kwanza uchunguzi au majaribio ya kina kuthibitishwa ni salama, lakini akili mnemba au AI imefikia watoto kupitia kusoma, urafiki au maswali binafsi ya msingi bila hata mtu mmoja kujiuliza athari mbaya za mfumo huo kwa watoto, amesema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres wakati wa ufunguzi wa Mjadala wa siku mbili kuhusu usimamizi wa akili mnemba ulioanza leo huko Geneva, Uswisi. Hivyo amesema, “hakuna mtoto anayepaswa kugeuzwa majaribio ya akili mnemba isiyodhibitiwa. Kwa kuendeleza kazi inayofanywa na Umoja wa Mataifa, nchi wanachama na wadau wengine, leo ninatoa wito wa kupitishwa kwa Ahadi ya Usalama wa Watoto katika Matumizi ya akili mnemba, yenye kanuni tatu rahisi kwa mfumo wowote wa AI unaoweza kufikiwa na watoto.”.Na taarifa ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Usafiri wa Baharini (IMO) iliyotolewa leo jijini London nchini Uingereza imemnukuu Katibu Mkuu wa shirika hilo, Arsenio Dominguez, akitoa wito wa hatua za haraka za kimataifa kuhakikisha mabaharia hao wanaachiliwa haraka na wakiwa salama. Taarifa ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Usafiri wa Baharini (IMO) iliyotolewa leo jijini London nchini Uingereza imemnukuu Katibu Mkuu wa shirika hilo, Arsenio Dominguez, akitoa wito wa hatua za haraka za kimataifa kuhakikisha mabaharia hao wanaachiliwa haraka na wakiwa salamaMwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
-
99
02 JULAI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina tunaangazia fursa ya kufanya mafunzo kwa vitendo au kwa lugha ya kiingereza Internship hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa. Rashid Malekela kutoka Mwanza Tanzania, ambaye aliomba na kupata fursa hiyo anazungumzia na Leah Mushi wa Idhaa hii kueleza ni nini faida yake.Mashirika ya misaada nchini Ukraine leo Alhamisi Julai 2 yameongeza juhudi za kutoa msaada kufuatia ongezeko kubwa la mashambulizi makubwa yaliyofanywa na Urusi usiku wa jana, yakiwemo yale yaliyolenga mji mkuu wa Ukraine, Kyiv na kuwa miongoni mwa mashambulizi makubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa dhidi ya mji huo.Mtaalamu wa Umoja wa Mataifa kuhusu ubaguzi wa zama za sasa Ashwini K.P ameonya kuwa ubaguzi wa rangi, chuki dhidi ya wageni, ubaguzi dhidi ya jamii za pembezoni, na aina nyingine za kutovumiliana zinazohusiana na misingi hiyo bado vimejikita kwa kina katika ngazi zote za michezo duniani. Kwenye ripoti yake kwa Baraza la Umoja wa Mataifa la haki za Binadamu, mtaalamu amesema michezo ina uwezo wa kukuza ujumuishi, usawa na mshikamano wa kijamii, lakini bado inaendelea kuakisi na kuendeleza mifumo ya ubaguzi wa rangi na kimaeneo unaoshuhudiwa katika jamii kwa ujumla.Na huko Mwanza, kaskazini-magharibi mwa Tanzania kumeanza mdahalo wa siku mbili wa vijana na amani ulioandaliwa na shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo, UNDP na mmoja wa washiriki anatoa maoni.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
-
98
Jifunze Kiswahili: Maana ya neno "MKUNGURU."
Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt. Mwanahija Ali Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anafafanua maana ya neno "MKUNGURU."
-
97
01 JULAI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina. Ikiwa ni siku chache baada ya maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Watu Wasioona na viziwi inayoadhimishwa tarehe 27 Juni kila mwaka, Rashid Malekela wa Idhaa hii anakupeleka Mashariki ya Kati akimmulika mkazi mwenye ulemavu ambaye anakumbwa na changamoto katikati ya vita.Wakati harakati za uokozi na usaidizi zikiendelea nchini Venezuela baada ya matetemeko mawili makubwa ya ardhi yaliyosababisha vifo vya watu zaidi ya 1700 hadi sasa, leo hii ikiwa ni siku ya saba Emily Camargo akiwa kwenye kituo cha hifadhi kilichoandaliwa na Umoja wa Mataifa jimboni La Guaira anaelezea alivyonusurika akisema, “kila kitu kilichonizunguka kiliporomoka na kunizingira, isipokuwa nilipokuweko. Nashukuru kwa sababu jengo la pembeni yetu halikuanguka. Hakuna kilichonipata. Hapa ndio tunalala, mimi, mume wangu , wifi yangu na mbwa wangu. Binadamu yangu na mpenzi wake hatujui waliko tumewatafuta hadi hospitalini, na kwenye orodha, hakuna dalili.”Jopo Huru la Kimataifa la Kisayansi la Umoja wa Mataifa kuhusu akili mnemba, limetoa ripoti leo inayoonesha kuwa teknolojia hiyo inaendelea kusonga mbele kwa kasi kubwa zaidi kuliko uwezo wa serikali kuandaa sera na kanuni zinazoendana nayo. Miaka michache iliyopita, akili mnemba ilikuwa ikitumika zaidi kujibu maswali au kuandika maandishi rahisi. Leo, teknolojia hii inaweza kutengeneza picha na video zenye uhalisia mkubwa na hata kufanya baadhi ya kazi bila usimamizi wa karibu wa binadamu lakini mifumo ya udhibiti na sheria za usalama haijafanikiwa kuendana na mabadiliko hayo.Baada ya miongo kadhaa hatimaye hii leo Umoja wa Mataifa umeondoa kanuni ya kifedha iliyokuwa ikiulazimisha kurejesha kwa nchi wanachama fedha ambazo hazikutumika hata kama fedha hizo hazikuwa zimewasilishwa kabisa. Uamuzi huo uliofanywa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa siku ya Jumanne unafuatia mapendekezo ya Kamati ya Tano, ya Baraza hilo ambayo inashughulikia masuala ya utawala na bajeti. Kanuni ilikwamisha ajira ndani ya Umoja wa Mataifa na operesheni za ulinzi wa amani. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, amesema kuwa kanuni hiyo ilikuwa inahatarisha uthabiti wa Umoja wa Mataifa na kwa uamuzi huu, Baraza limeanzisha mbinu mpya itakayohakikisha kuwa fedha ambazo hazijatumika zinarejeshwa kwa nchi wanachama pale tu zinapokuwa zimewasilishwa taslimu na kupokelewa.Na katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anafafanua maana ya neno "MKUNGURU."Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
-
96
30 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inayoangazia sekta ya ufugaji wa samaki na viumbe vingine na mimea baharini na kwenye maziwa, sekta ambayo inaendelea kushuhudia ukuaji mkubwa duniani, huku uzalishaji wa samaki ukifikia kiwango cha juu zaidi kuwahi kurekodiwa.Shughuli za uokoaji zinaendelea nchini Venezuela kufuatia athari za matetemeko makubwa ya ardhi yaliyoua maelfu ya watu na kuwaacha maelfu wengine bila makazi. Mashirika ya Umoja wa Mataifa yalipozungumza na waandishi wa habari leo jijini Geneva, Uswisi yametahadharisha kuwa uhaba wa huduma za afya, chakula na makazi unaongeza hatari ya milipuko ya magonjwa. Msemaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani, WHO, Christian Lindmeier amesisitiza wawasi huo akisema “Huduma za afya ziko chini ya shinikizo kubwa sana kwa sasa.”Tathmini mpya ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo, UNDP imeonya kuwa mlipuko wa Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC unaweza kuwasukuma karibu watu milioni moja zaidi kuingia kwenye umaskini, huku wanawake wakitarajiwa kuathirika zaidi kiuchumi na kiafya. Ripoti hiyo iliyotolewa leo New York Marekani na Kinshasa, DRC pia inaeleza kuwa mlipuko huu wa sasa unaweza kugharimu uchumi wa Afrika hadi dola bilioni 3.6 za Marekani iwapo athari zake zitaenea zaidi.Na, Kuelekea Mdahalo wa kwanza wa Kimataifa Kuhusu Usimamizi wa Akili Mnemba, AI utakaofanyika wiki ijayo jijini Geneva, Uswisi, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto, UNICEF limezitaka serikali na wadau kuhakikisha haki za watoto zinazingatiwa katika usimamizi wa matumizi ya akili mnemba (AI). Shirika hilo linataka sheria madhubuti za kuzuia unyanyasaji wa watoto unaowezeshwa na AI, mifumo ya AI iliyo salama na yenye uwazi, pamoja na uwekezaji katika utafiti, elimu ya matumizi ya AI.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
-
95
29 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inayokupeleka mjini Caracas nchini Venezuela, mshikamano na raia wa nchi hiyo wadhihirika wakati huu wakiwa kwenye majonzi baada ya matetemeko ya ardhi kukumba wananchi. Pia tunakuletea muhtasari wa habari kama zifuatazo.Nchini Venezuela Mashirika ya Umoja wa Mataifa yanaendelea kutoa msaada kufuatia matetemeko mawili ya ardhi yaliyolikumba taifa hilo wiki iliyopita. Mathalani, Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani, WFP, limeripoti leo kwamba tayari limetoa zaidi ya tani elfu tatu za chakula, kiasi kinachotosha kusaidia familia zaidi ya elfu kumi kwa kipindi cha miezi miwili.”Huko mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia Congo DRC, raia wameelezea haki zao zinazokiukwa ikiwemo kuzuiwa kupatiwa misaada ukatili wa kingono na mauaji. Maelezo hayo yamo kwenye ripoti iliyotolewa leo na Tume Huru ya Umoja wa Mataifa inayochunguza hali ya haki za binadamu katika majimbo ya Kivu Kaskazini na Kivu Kusini, ikiwa ni ripoti yao ya kwanza mbele ya Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa mjini Geneva, Uswisi?”.Na, michuano ya Fainali ya Kombe la Dunia la Mpira wa Miguu inaendelea huku dunia ikishuhudia ongezeko la joto kali. Katika juhudi za kulinda wachezaji, wafanyakazi na mashabiki dhidi ya athari za joto, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya duniani WHO, Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus amesema “WHO tunashirikiana na FIFA na nchi zinazoandaa michuano hiyo katika kampeni iitwayo Beat the Heat inayolenga kuweka mipango ya utekelezaji, kutoa elimu kwa wananchi, kuanzisha mifumo ya tahadhari za mapema, kuboresha upatikanaji wa maji salama ya kunywa, pamoja na kuweka maeneo ya kujipooza.”Mwenyeji wako ni Rashid Malekela, karibu!
-
94
Jifunze Kiswahili: Maana ya methali “Lengelenge lako si jipu langu.”
Katika kujifunza lugha ya Kiswahili, tunasalia huko huko Nairobi Kenya kwani leo mchambuzi wetu ni Dkt. Josephat Gitonga, ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi, kwenye kitivo cha Tafsiri na Ukalimani anafafanua maana ya methali “Lengelenge lako si jipu langu”.
-
93
26 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inayokupeleka jijini Nairobi nchini Kenya ambako kunafanyika Mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Intaneti, IGF, mahususi kwa bara la Afrika pekee, AfIGF. Stella Vuzo, Afisa Habari wa UNIS Nairobi, Kenya amezungumza na mmoja wa vijana washiriki na kukuletea maoni yake.Idadi ya waliokufa kwenye matetemeko mawili makubwa ya ardhi yaliyokumba Venezuela wiki hii ikiongezeka na kufikia 235, afisa wa shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji IOM nchini humo Luis Segovia akizungumza kutoka mji mkuu Caracas baada kusambaza vifaa vya dharura kwa familia amesema, “leo, IOM itaendelea kufanya kazi kwa karibu na mamlaka husika pamoja na washirika wa kibinadamu ili kuhakikisha msaada unawafikia kwa wakati wale wanaouhitaji zaidi.”Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, waambata wa wagonjwa au watu waliokufa kwa Ebola wakishindwa kusalia kwenye karantini ili kudhibiti kusambaa kwa ugonjwa huo, David Stevenson, Mwakilishi Mkazi wa shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula WFP kupitia ukurasa wa X amesema ni muhimu kuongeza usaidizi wa shirika hilo ili liweze kutoa mgao zaidi kwa wahitaji waliko, akitoa mfano wa swali alilosema rahisi lakini chungu kutoka kwa mkimbizi wa ndani Jack aliyefiwa na mwanae kwa Ebola na mkewe yuko karantini, na sasa analea watoto 13 kwa msaada wa mgao wa chakula kutoka WFP. “Kwa watoto wote hawa, mgao huu wa chakula wa mwezi mmoja utadumu kwa wiki mbili tu. Na baada ya hapo, nitawalishaje ilhali sina njia yoyote ya kufanya hivyo?”.Ripoti ya mwaka huu wa 2026 kuhusu dawa za kulevya na uhalifu imeonya kuhusu ongezeko la dawa mpya za kutengenezwa maabara huku maendeleo ya teknolojia yakiwezesha wasafirishaji kukwepa kubainika. Mkurugenzi Mtendaji wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kudhibiti Dawa za Kulevya na Uhalifu, (UNODC) Monica Juma, amesema dunia inashuhudia ongezeko ambalo halijawahi kutokea la aina mpya za dawa za kulevya, huku baadhi zikiwa na nguvu na hatari zaidi kuliko zilizokuwepo awali.Na katika kujifunza lugha ya Kiswahili, tunasalia huko huko Nairobi Kenya kwani leo mchambuzi wetu ni Dkt. Josephat Gitonga, ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi, kwenye kitivo cha Tafsiri na Ukalimani anafafanua maana ya methali “Lengelenge lako si jipu langu”.Mwenyeji wako ni Feissal Kirwa, karibu!
-
92
Tunataka wasichana nchini DRC wasahau machungu ya vita na kuanza maisha mapya: Lydie Mwenge
Katika mji wa Goma mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), ambako miongo ya vita imeacha maelfu ya watoto bila familia, elimu au usalama, Lydie Mbusa Mwenge ameweka maisha yake katika mstari wa mbele wa kupigania haki za wasichana walioathiriwa na vita. Mwenge ni mwanzilishi na mratibu wa shirika la Action Intervention des Femmes Entrepreneurs pour le Développement, linalojikita katika kulinda na kuwawezesha wasichana walio chini ya umri wa miaka 18, hususan wale manusura wa ubakaji, kupoteza familia zao au kulazimika kuishi mitaani. Bi. Lydie Mwenge amezungumza na Flora Nducha wa Idhaa hii, ungana nao.
-
91
25 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina, leo tunaelekea nchini DRC, kwa Lydie Mwenge, Mwanaharakati wa kupigania haki hususan za wasichana walio na umri wa chini ya miaka 18 walioathirika na vita inayoendelea nchini humo ukiwemo ukatili wa kingono.Mashirika ya Umoja wa Mataifa yanaendelea na harakati za kutoa msaada wa dharura kwa Venezuela kufuatia matetemeko mawili makubwa ya ardhi yaliyolikumba taifa hilo jana Jumatano Juni 24, na kusababisha vifo vya watu wasiopungua 164 pamoja na uharibifu mkubwa katika mji mkuu, Caracas, na maeneo ya jirani. Matetemeko hayo mawili yenye ukubwa wa 7.2 na 7.5 katika kipimo cha Richter yametokea ndani ya muda wa chini ya dakika moja, yakiharibu nyumba, hospitali, barabara na miundombinu mingine muhimu.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, ametoa wito wa kuimarishwa kwa ulinzi wa mabaharia duniani, akionya kuwa ongezeko la migogoro na mivutano ya kisiasa linaweka maelfu ya wafanyakazi wa baharini katika hatari wakati wakiendelea kuhakikisha biashara na usafirishaji wa bidhaa duniani vinaendelea. Katika ujumbe wake wa kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Mabaharia, inayoadhimishwa kila mwaka tarehe 25 Juni, Katibu Mkuu amesema karibu asilimia 90 ya bidhaa na mahitaji muhimu duniani, ikiwemo chakula, dawa na nishati, husafirishwa kwa njia ya bahari.Na maandalizi ya Mkutano wa 15 wa Afrika Kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Intaneti, AfIGF utakaofanyika mwezi Novemba mwaka huu nchini Ghana yameanza ambapo maoni ya wadau yatakusanywa ili kuweka mazingira salama ya matumizi ya intaneti barani Afrika na hatimaye duniani. Vijana na watoto kutoka nchi mbalimbali wamekutana jijini Nairobi Kenya kuandaa mawazo yao na mmoja wao ni Sheryl Christine Adhiambo kutoka taasisi ya Legal Sisters ya nchini Kenya.Mwenyeji wako ni Feissal Kirwa, karibu!
-
90
Papa Leo XIV: Juhudi na mshikamano wa kimataifa ni kiini cha kutokomeza njaa
Katika kipindi ambacho idadi ya watu wanaokabiliwa na njaa duniani inaendelea kuongezeka kutokana na migogoro, mabadiliko ya tabianchi na changamoto za kiuchumi, kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Leo wa Kumi na Nne (Leo XIV), ametuma ujumbe wa mshikamano kwa kutembelea makao makuu ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani, WFP, mjini Roma nchini Italia wiki hii. Ziara hiyo imeangazia umuhimu wa kuimarisha juhudi za kimataifa katika mapambano dhidi ya njaa. Flora Nducha na taarifa zaidi
-
89
UN yathibitsha zaidi ya matukio 500 ya ukatili wa kijinsia nchini Sudan
Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu, OHCHR, imetoa ripoti kuhusu ongezeko kubwa la ukatili wa kingono unaohusiana na mzozo nchini Sudan tangu mapigano yalipoanza zaidi ya miaka mitatu iliyopita. Ofisi hiyo imekumbusha jumuiya ya kimataifa umuhimu wa kuhakikisha haki na uwajibikaji vinapewa kipaumbele wakati juhudi za kusitisha mapigano na kutafuta suluhu ya mzozo huo zikiendelea. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Selina Jerobon.
-
88
24 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunaangazia usalama wa mabaharia katika Mlango Bahari wa Hormuz, ongezeko kubwa la ukatili wa kingono unaohusiana na mzozo nchini Sudan, na ujumbe wa Papa Leo wa Kumi na Nne (Leo XIV), kuhusu ongezeko la njaa duniani.Shirika la Umoja wa Mataifa la Usafiri wa Baharini (IMO) limetangaza mpango wa kuwaondoa zaidi ya mabaharia 11,000 waliokwama katika Mlango Bahari wa Hormuz kufuatia makubaliano ya amani kati ya Iran na Marekani yaliyolenga kurejesha usalama wa usafiri wa baharini katika eneo hilo. Anold Kayanda amefuatilia hatua hiyo.Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu, OHCHR, imetoa ripoti kuhusu ongezeko kubwa la ukatili wa kingono unaohusiana na mzozo nchini Sudan tangu mapigano yalipoanza zaidi ya miaka mitatu iliyopita. Ofisi hiyo imekumbusha jumuiya ya kimataifa umuhimu wa kuhakikisha haki na uwajibikaji vinapewa kipaumbele wakati juhudi za kusitisha mapigano na kutafuta suluhu ya mzozo huo zikiendelea.Katika kipindi ambacho idadi ya watu wanaokabiliwa na njaa duniani inaendelea kuongezeka kutokana na migogoro, mabadiliko ya tabianchi na changamoto za kiuchumi, kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Leo wa Kumi na Nne (Leo XIV), ametuma ujumbe wa mshikamano kwa kutembelea makao makuu ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani, WFP, mjini Roma nchini Italia wiki hii. Ziara hiyo imeangazia umuhimu wa kuimarisha juhudi za kimataifa katika mapambano dhidi ya njaa.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
-
87
IMO yatangaza mpango wa kuwaondoa mabaharia waliokwama Hormuz
Shirika la Umoja wa Mataifa la Usafiri wa Baharini (IMO) limetangaza mpango wa kuwaondoa zaidi ya mabaharia 11,000 waliokwama katika Mlango Bahari wa Hormuz kufuatia makubaliano ya amani kati ya Iran na Marekani yaliyolenga kurejesha usalama wa usafiri wa baharini katika eneo hilo. Anold Kayanda amefuatilia hatua hiyo. Karibu Anold utufahamishe zaidi.
-
86
Jifunze Kiswahili: Maana za neno "TANUWINI"
Katika kujifunza lugha ya Kiswahili hii leo mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana za neno "TANUWINI"
-
85
23 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inayoturejesha hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa ambapo Leah Mushi ameketi chini na Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Nassriya Nassir Ali akieleza safari yake ya uongozi wa nafasi za umma kupitia mkalimani wake wa lugha ya alama Tusajigwa Ernest. Pia tunakuletea Muhtasariw a habari na jifunze Kiswahili.Janga la tabianchi linakaribia kwa kasi zaidi kuliko inavyodhaniwa ameonya leo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, huku akitoa wito wa hatua saba za haraka kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi na kuachana na matumizi ya mafuta ya kisukuku. Akizungumza mjini London kwenye mkutano wa hatua dhidi ya tabianchi, ametaja hatua hizo kuwa ni pamoja na Serikali zichukue hatua madhubuti za tabianchi, dunia iongeze matumizi ya nishati safi, ilinde jamii zilizo hatarini, ihakikishe ufadhili wa haki kwa nchi zinazoendelea, isimamie kwa uwajibikaji matumizi ya teknolojia ya akili mnemba na kupambana na upotoshaji wa taarifa kuhusu tabianchi. Guterres amesema hatua hizo ni muhimu ili kudhibiti ongezeko la joto duniani na kuzuia madhara makubwa zaidi kwa binadamu na mazingira.Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi, UNHCR, limekaribisha makubaliano mapya kati ya DRC na Rwanda ya kusaidia wakimbizi kurejea nyumbani kwa hiari, usalama na heshima. Katika mkutano uliofanyika Addis Ababa Ethiopia, serikali za nchi hizo mbili zimeahidi kuimarisha ushirikiano kwa msaada wa UNHCR ili kuwezesha urejeaji salama wa wakimbizi.Zaidi ya wagonjwa 1,000 vya Ebola wamethibitishwa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC, huku watu 254 wakifariki dunia kwa mujibu wa Shirika la Afya la Umoja wa Mataifa Duniani WHO likiongeza kuwa wagonjwa 100 wamepona, jambo linaloonesha kuwa huduma ya afya ya haraka inaweza kuokoa maisha.Na katika kujifunza lugha ya Kiswahili hii leo mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana za neno "TANUWINI"Mwenyeji wako ni Feissal Kirwa, karibu!
-
84
22 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina. Hivi karibuni Shirika la Umoja wa Mataifa la Kupambana na UKIMWI, UNAIDS kupitia ripoti yake mpya limeonya kuwa kupungua kwa ufadhili wa kimataifa na uwekezaji mdogo katika huduma za kinga dhidi ya Virusi vya UKIMWI, VVU kunaweza kufuta mafanikio yaliyopatikana katika mapambano dhidi ya UKIMWI duniani.Katika hatua za mwitikio wa kitaifa, wiki iliyopita, Tume ya Kudhibiti UKIMWI nchini Tanzania, TACAIDS kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto, UNICEF nchini humo imeendesha warsha ya siku tano kuanzia Juni 15 hadi 19 kwa ajili ya kuwajengea uwezo viongozi wa asasi za vijana na wawakilishi wa vijana katika utetezi wa masuala ya VVU na Afya ya Uzazi. Pia tunakuletea Muhtasariw a habari.Leo katika Makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani, viongozi wa dunia wanakutana katika Mkutano wa Ngazi ya Juu kuhusu Virusi vya UKIMWI VVU, na UKIMWI kujadili mafanikio na changamoto za mapambano dhidi ya janga hilo tangu mwaka 2021. Mkutano huo unaofanyika kila baada ya miaka mitano unalenga kupitisha Azimio jipya la Kisiasa litakaloelekeza hatua za dunia katika kukabiliana na UKIMWI kwa miaka mitano ijayo.Shirika la Umoja wa Mataifa la masuala ya wanawake, UN Women, limeonya kuwa matumizi ya akili mnemba au AI yanaongeza hatari ya ubaguzi dhidi ya wanawake na wasichana duniani. Utafiti wa mifumo 133 ya AI umebaini kwamba asilimia 44 ilikuwa na upendeleo wa kijinsia, huku asilimia 26 ikiwa na ubaguzi wa kijinsia na rangi kwa pamoja.Na Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC, hatua za kujikinga dhidi ya Ebola zimeimarishwa katika Gereza Kuu la Bunia ambako zaidi ya wafungwa 2,000 wanaishi katika mazingira ya msongamano mkubwa. Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani, WHO kanda ya Afrika, kwa ushirikiano na ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO, wamejenga kituo maalum cha muda cha kutenga wagonjwa wa Ebola.Mwenyeji wako ni Feissal Kirwa, karibu!
-
83
19 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunaangazia wito wa UN wa kulinda mamilioni wa wakimbizi kote duniani, masuala ya kijinsia Zanzibar nchini Tanzania, na ripoti mpya ya Katibu Mkuu wa UN kuhusu watoto katika maeneo ya machafuko imeonesha hali ya kutisha duniani.Kuelekea maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wakimbizi kesho Juni 20, viongozi wa Umoja wa Mataifa wametoa wito wa kuimarishwa kwa mshikamano na hatua za kimataifa za kuwalinda mamilioni ya watu waliolazimika kuyakimbia makazi yao kote duniani kutokana na vita, vurugu na mateso.Ripoti mpya ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu watoto katika maeneo ya machafuko imeonesha hali ya kutisha duniani. Takribani watoto 24,174 waliuawa, kujeruhiwa, kulazimishwa kujiunga na makundi yenye silaha, kubakwa au kuathiriwa kwa namna nyingine na ukiukwaji mkubwa wa haki katika maeneo yenye mizozo mwaka 2025.Je, maisha yangekuwaje kama kila manusura wa ukatili wa kijinsia angejua mahali pa kupata msaada kwa wakati? Kisiwani Zanzibar nchini Tanzania Shirika la Umoja wa Mataifa la Masuala ya Wanawake (UN Women), kwa ufadhili wa Muungano wa Ulaya (EU) na kwa ushirikiano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, linaimarisha upatikanaji wa haki na huduma za msaada kwa manusura wa ukatili wa kijinsia, hususan katika maeneo ya pembezoni. Kupitia mradi wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Wasichana Zanzibar na Kuimarisha Uongozi wa Wanawake, manusura wanapata habari muhimu, ushauri nasaha na msaada wa kisheria wakati wowote.Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
-
82
UN yataka dhamira mpya wakati takriban wakimbizi milioni 42 duniani wakiendelea kuhitaji ulinzi
Kuelekea maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wakimbizi kesho Juni 20, viongozi wa Umoja wa Mataifa wametoa wito wa kuimarishwa kwa mshikamano na hatua za kimataifa za kuwalinda mamilioni ya watu waliolazimika kuyakimbia makazi yao kote duniani kutokana na vita, vurugu na mateso. Anold Kayanda amefuatilia na kutuandalia taarifa ifuatayo.
-
81
Mauaji na majeraha ya watoto yafikia kiwango cha kutisha duniani - UN
Ripoti mpya ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu watoto katika maeneo ya machafuko imeonesha hali ya kutisha duniani. Takribani watoto 24,174 waliuawa, kujeruhiwa, kulazimishwa kujiunga na makundi yenye silaha, kubakwa au kuathiriwa kwa namna nyingine na ukiukwaji mkubwa wa haki katika maeneo yenye mizozo mwaka 2025. Leah Mushi amemsikiliza Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Watoto katika Maeneo ya Migogoro ya Silaha, akizungumzia ripoti hiyo, na kutuandalia taarifa ifuatayo.
-
80
UN Women na EU waleta matumaini kwa wanawake waathirika wa ukatili viziwani Zanzibar
Je, maisha yangekuwaje kama kila manusura wa ukatili wa kijinsia angejua mahali pa kupata msaada kwa wakati? Kisiwani Zanzibar nchini Tanzania Shirika la Umoja wa Mataifa la Masuala ya Wanawake (UN Women), kwa ufadhili wa Muungano wa Ulaya (EU) na kwa ushirikiano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, linaimarisha upatikanaji wa haki na huduma za msaada kwa manusura wa ukatili wa kijinsia, hususan katika maeneo ya pembezoni. Kupitia mradi wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Wasichana Zanzibar na Kuimarisha Uongozi wa Wanawake, manusura wanapata habari muhimu, ushauri nasaha na msaada wa kisheria wakati wowote. Feissal Kirwa na taarifa zaidi.
-
79
18 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina. Katika mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu uliomalizika wiki iliyopita baadhi ya wahudhuriaji walikuja na wakalimani wao, kutoka Tanzania Mbunge Nassriya Nassir Ali mwenye ulemavu wa kusikia au Kiziwi aliambatana na mkalimani wake Tusajigwe Ernest. Baada ya mkutano huo Leah Mushi aliketi na Tusajigwe na hapa anaanza kwa kueleza kuhusu taaluma yake. Pia tunakuletea muhtasari wa habari.Kauli za chuki zinaendelea kuhatarisha mshikamano wa jamii na amani duniani, ameonya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres akisema mara nyingi ndizo chachu ya vurugu, migogoro na uhalifu mkubwa dhidi ya ubinadamu. Katika ujumbe wake wa Siku ya Kimataifa ya Kupambana na Kauli za Chuki, leo Juni 18, Guterres amesema makundi kama wanawake, wahamiaji, wakimbizi, watu wenye ulemavu na jamii ya LGBTQIA+ mara nyingi hulengwa na ujumbe wa chuki. “Kauli za chuki ndio hatua ya kwanza katika njia ya kuwanyima watu utu wao, njia ambayo mara nyingi hupelekea vurugu, migogoro na uhalifu wa kutisha.” Pia ameonya kuwa mitandao ya kijamii imeongeza kasi ya kusambaa kwa chuki duniani.Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa Kulinda Amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, MONUSCO, umetangaza kwa masikitiko hii leo kifo cha mfanyakazi wa kampuni iliyokuwa ikitoa huduma kwa ujumbe huo, aliyefariki dunia kutokana na Ebola mjini Bunia. MONUSCO imesema mfanyakazi huyo alikuwa ameacha kufanya kazi na ujumbe huo tangu Mei 22 mwaka huu na hakuwa amefika katika maeneo ya MONUSCO kwa zaidi ya siku 21 kabla ya ugonjwa huo kuthibitishwa. Ujumbe huo umetuma salamu za rambirambi kwa familia, ndugu, marafiki na wafanyakazi wenzake na marehemu.Na Shirika la Umoja wa Mataifa la Hali ya Hewa Duniani, WMO, limesema matukio mabaya ya hali ya hewa na mabadiliko ya tabianchi yaliathiri takriban watu milioni 13 barani Afrika mwaka 2025 na kusababisha vifo zaidi ya watu 3,000. Ripoti mpya ya shirika hilo iliyotolewa leo mjini Geneva Uswisi inaeleza kuwa mafuriko yalikuwa janga lililoripotiwa zaidi, huku yakisababisha hasara kubwa za kiuchumi na kibinadamu. WMO pia imeonya kuwa barafu katika maeneo ya milima ya Afrika, ikiwemo Mlima Kilimanjaro, inaendelea kutoweka kwa kasi, wakati kina cha bahari katika baadhi ya maeneo ya pwani kikipanda kwa kiwango kikubwa kuliko wastani wa dunia. WMO imesisitiza kuwa Afrika bado ina pengo kubwa katika mifumo ya tahadhari za mapema, ingawa maendeleo yanaendelea kufanyika.Mwenyeji wako ni Feissal Kirwa, karibu!
-
78
Vijana wanahitaji ajira, stadi na matumaini bila hivyo, ni rahisi kutumbukia kwenye uhalifu - Monica Juma
Wakati dunia ikikabiliwa na ongezeko la uhalifu wa kupangwa, biashara haramu ya binadamu na matumizi ya dawa za kulevya, mwanamke kutoka Afrika Mashariki amepewa jukumu kubwa la kusaidia kuongoza mapambano ya kimataifa dhidi ya changamoto hizo. Monica Juma, ambaye hivi karibuni ameteuliwa kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Dawa za Kulevya na Uhalifu (UNODC), anavunja rekodi kwa kuwa mwanamke wa kwanza kutoka Afrika Mashariki na Kusini mwa dunia kushika nafasi hiyo ya juu katika taasisi hiyo ya Umoja wa Mataifa. Pata mahojiano maalum na ya kina baina ya Flora Nducha wa Idhaa hii na Mkuu huyu mpya wa ofisi ya UNODC.
-
77
Watoto 9 waliotumikishwa kijeshi na waasi waachiwa na kuanza maisha mapya nchini Sudan Kusini
Watoto tisa waliokuwa wakihusishwa na vikosi vya ulinzi katika Jimbo la Equatoria Magharibi nchini Sudan Kusini wameanza safari mpya ya maisha baada ya kutambuliwa, kuachiliwa na kukabidhiwa kwa ajili ya kurejeshwa katika familia na jamii zao.
-
76
Mashirika ya UN FAO na WFP waonya kuongezeka kwa njaa kali kwenye maeneo 13 duniani
Mashirika ya Umoja wa Mataifa lile la Chakula na Kilimo, FAO, pamoja na Mpango wa Chakula Duniani, WFP, yametoa onyo kali kuwa hali ya ukosefu wa uhakika wa chakula inatarajiwa kuwa mbaya zaidi kwa mamilioni ya watu katika nchi 13 zilizotajwa kuwa maeneo hatari ya njaa kati ya mwezi Juni na Novemba mwaka huu wa 2026. Anold Kayanda ameifuatilia taarifa hiyo.
-
75
17 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunaangazia uhakika wa chakula barani Afrika, utumikishaji wa watoto jeshini Sudan Kusini, na ujumbe wa mwanaharakati wa haki za wanawake na wasichana kutoka asasi ya kiraia nchini Zimbabwe.Mashirika ya Umoja wa Mataifa lile la Chakula na Kilimo, FAO, pamoja na Mpango wa Chakula Duniani, WFP, yametoa onyo kali kuwa hali ya ukosefu wa uhakika wa chakula inatarajiwa kuwa mbaya zaidi kwa mamilioni ya watu katika nchi 13 zilizotajwa kuwa maeneo hatari ya njaa kati ya mwezi Juni na Novemba mwaka huu wa 2026.Watoto tisa waliokuwa wakihusishwa na vikosi vya ulinzi katika Jimbo la Equatoria Magharibi nchini Sudan Kusini wameanza safari mpya ya maisha baada ya kutambuliwa, kuachiliwa na kukabidhiwa kwa ajili ya kurejeshwa katika familia na jamii zao.Leo tunakupeleka Zimbabwe kwa mwanaharakati wa haki za wanawake na wasichana kutoka asasi ya kiraia ya “Unlimited Hope Alliance”. Kandoni mwa moja ya mikutano ya Zama Zijazo ya Umoja wa Mataifa hapa New York Marekani alipata fursa ya kuzungumza na Flora Nducha wa Idhaa hii akipaza sauti kwa viongozi wa dunia kuhakikisha wanawake na wasichana wa vijijini hawapewi kisogo katika ajenda za maendeleo, elimu na teknolojia.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
-
74
Hata kama ulipata mimba ukiwa na umri wa miaka 14 huo sio mwisho wa maisha yako - Mary Chigumira
Leo tunakupeleka Zimbabwe kwa mwanaharakati wa haki za wanawake na wasichana kutoka asasi ya kiraia ya “Unlimited Hope Alliance”. Kandoni mwa moja ya mikutano ya Zama Zijazo ya Umoja wa Mataifa hapa New York Marekani alipata fursa ya kuzungumza na Flora Nducha wa Idhaa hii akipaza sauti kwa viongozi wa dunia kuhakikisha wanawake na wasichana wa vijijini hawapewi kisogo katika ajenda za maendeleo, elimu na teknolojia. Flora Nducha anafafanua zaidi alichomueleza katika taarifa hii
-
73
16 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inayoturejesha hapa Makao Makuu ya UN kusikia mahojiano maalum na ya kina baina ya Flora Nducha wa Idhaa hii na Mkuu mpya wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Dawa na Uhalifu UNODC. Pia tunakuletea Muhtasari wa habari.Kumekuwepo na imani kwamba ugonjwa wa Ebola si halisi, hali iliyowafanya baadhi ya wananchi nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, kuzika wapendwa wao waliokufa kwa Ebola bila kufuata hatua za kujikinga dhidi ya maambukizi. Kutafuta suluhu ya changamoto hiyo, Shirika la Afya Duniani WHO kwa kushirikiana na Shirikisho la Kimataifa la chama cha Msalaba Mwekundu na Hilali Nyekundu, IFRC, wamesikiliza maoni ya jamii kuhusu taratibu za mazishi.Takriban nusu ya watoto wote duniani au watoto bilioni 1.1 sasa wanakabiliwa na angalau hatari tatu za mabadiliko ya tabianchi zinazolingana, zikihatarisha afya zao, elimu, na maisha yao, imesema ripoti iliyotolewa leo na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto UNICEF.Na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, yuko nchini Haiti kwa ziara maalum ya mshikamano ili kujionea hali halisi ya wananchi walioathiriwa na ghasia na ukosefu wa usalama. Akiwa huko, Guterres anakutana na wananchi, kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa Haiti, na kutathmini juhudi za serikali, Umoja wa Mataifa na jumuiya ya kimataifa za kurejesha utulivu nchini humo.Mwenyeji wako ni Feissal Kirwa, karibu!
-
72
15 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inayotupeleka nchini Kenya kufuatilia ziara ya kihistoria ya Rais wa Baraza Kuu la UN, Annalena Baerbock, kwenye kituo cha kukusanya, kuchakata na kurejeleza taka cha Korogocho (Korogocho Material Recovery Facility - MRF) kujionea namna vijana wanavyogeuza taka kuwa fursa ya kiuchumi na silaha ya kutokomeza umasikini na uhalifu mitaani.Kufuatia makubaliano ya sitisho la mapigano la kudumu baina ya Marekani na Iran yaliyotangazwa jana jumapili Juni 14, viongozi wa ngazi za juu wa Umoja wa Mataifa wampongeza kufikiwa kwa makubaliano hayo huku wakihimiza yaheshimiwe na pia kufunguliwe upenyo maalum wa kupitisha misaada ya kibinadamu katika mlango bahari wa Hormuz huko nchini Iran.Kutoka Mashariki ya Kati twende Afrika, ambako mapigano nchini Sudan yanaelezwa kutoonesha dalili yoyote ya kupungua, huku pande zinazohasimiana zikituhumiwa kutumia mbinu za kukamatwa kiholela, mateso na kutoweshwa kwa raia kwa nguvu. Taarifa iliyotolewa leo na Tume Huru ya Umoja wa Mataifa ya Kuchunguza Ukweli kuhusu Sudan imesema vitendo hivyo vinaweza kuhesabiwa kuwa uhalifu dhidi ya ubinadamu.Na leo ni Siku ya siku ya Uelimishaji Kuhusu Ukatili dhidi ya Wazee Duniani ambapo Umoja wa Mataifa umesema hatua zaidi zinahitajika kuwalinda wazee dhidi ya ukatili, huku ukionya kuwa uelimishaji pekee hautoshi na kwamba dunia inapaswa kuimarisha sheria, huduma za afya na mifumo ya kuripoti matukio ya unyanyasaji.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
-
71
12 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina. Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu CRPD, umehitimishwa jana katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani. Watu wenye ulemavu na wadau mbalimbali wa Serikali na Mashirika yasiyo ya Serikali walikusanyika kutoka kila pembe ya dunia kujadili hatua zilizopigwa katika kipindi cha miaka 20 ya Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Watu Wenye Ulemavu, CRPD. Mmoja wa waliohudhuria ni Bwana Kibaya Laibuta ambaye licha ya kupoteza uwezo wa kuona akiwa na umri wa miaka 24 alipokuwa mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha Nairobi bado alifanikiwa kusonga mbele akamaliza masomo yake ya sheria na masomo mengine ya ngazi za juu na sasa miaka mingi baadaye ni Jaji katika Mahakama ya Rufaa ya Kenya. Siri yake ya mafaniko ndio hasa anaihamasisha kote duniani na anaiweka wazi katika mazungumzo yafuatayo na Anold Kayanda wa Idhaa hii ya Umoja wa Mataifa ili watu wengine wenye ulemavu wafanikiwe kama yeye. Pia tunakuletea muhtasari wa habari zikiwemo za hatua za kupambana na UKIMWI, maambukizi ya ugonjwa wa Ebola hasa kwa watoto DRC, na ujumbe katika siku ya kimataifa ya kupinga utumikishaji wa watoto.Mwenyeji wako ni Rashid Malekela.
-
70
Jifunze Kiswahili: Maana ya methali “Lililo lujani ni la lusu”
Katika kujifunza lugha ya Kiswahili, leo mchambuzi wetu ni Dkt. Josephat Gitonga, ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi nchini Kenya kwenye kitivo cha Tafsiri na Ukalimani anafafanua maana ya methali “Lililo lujani ni la lusu”.
-
69
11 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina. Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu CRPD, umetamatishwa leo katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani. Idhaa hii imepata fursa ya kuzungumza na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya mkutano huu muhimu, Mtanzania Zuleikha Tambwe. Pia tunakuletea jifunze Kiswahili na muhtasari wa habari kama zifuatazo..Hatari ya Ebola wakati wa Kombe la Dunia la Soka 2026 ni ndogo na hakuna sababu ya mashabiki kubadili mipango yao ya safari kuelekea Canada, Mexico na Marekani, limesema Shirika la Afya Duniani WHO kombe hilo liking’oa nanga leo. Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Ulaya, Hans Henri P. Kluge, amesema hakuna wagonjwa wa Ebola katika nchi hizo wala Ulaya na amesisitiza, “Safirini kama kawaida na furahieni mashindano hayo.” WHO imefafanua kuwa Ebola haisambai kwa njia ya hewa na visa vingi vipo katika maeneo ya mbali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Annalena Baerbock, amehitimisha ziara ya siku mbili jijini Nairobi nchini Kenya, ambapo amesisitiza nafasi muhimu ya Umoja wa Mataifa katika kuendeleza maendeleo, amani na ushirikiano barani Afrika. "Kila siku Umoja wa Mataifa na washirika wake huokoa maisha. Bila UN, mamilioni ya watoto wasingepata elimu kupitia UNICEF wala chanjo muhimu kupitia WHOna tusingekuwa na ushirikiano kama huu."Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu CRPD, uliokuwa unafanyika hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani umefikia tamati leo. Kaulimbiu ya mwaka huu ni “kuadhimisha miaka 20 ya mkataba huo na kuimarisha utekelezaji wake katika dunia inayobadilika.” Kibaya Laibuta, Jaji wa Mahakama ya Rufani nchini Kenya, ambaye pia ni mlemavu aliyeoona au kipofu, ameshiriki na anaeleza alivyouona mkutano huu.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili, leo mchambuzi wetu ni Dkt. Josephat Gitonga, ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi nchini Kenya kwenye kitivo cha Tafsiri na Ukalimani anafafanua maana ya methali “Lililo lujani ni la lusu”.Mwenyeji wako ni Rashid Malekela, karibu!
-
68
10 JUNI 2026
Jaridani leo tunakuletea mada kwa kina maalum ambayo kama nilivyokujuza hapo awali inaangazia mkutano wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu CRPD, unaofanyika hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa chini ya kauli mbiu “kuadhimisha miaka 20 ya mkataba huo na kuimarisha utekelezaji wake katika dunia inayobadilika.”Washiriki wanajadili namna ya kutokomeza ukandamizaji, ukatili na manyanyaso dhidi ya watu wenye ulemavu, kuimarisha mifumo ya huduma na msaada, pamoja na kuongeza ushiriki na uwakilishi wao katika maisha ya kisiasa na umma. Miongoni mwa wanaohudhuria mkutano huo ni Nassriya Nassir Ali mbunge wa watu wenye ulemavu kutoka nchini Tanzania, yeye anaulemavu wa kusikia au kiziwi. Leah Mushi amefanya mahojiano naye na hapa mkalimani wake wa lugha ya Alama Tusajigwe Ernest anajibu kwa sauti. Pia tunakuletea mhtasari wa habari tukimulika haki za elimu kwa watoto nchini Sudan, usalama wa mabaharia na judhibiti wa kusambaa kwa virusi vya Ebola hasa wakati huu wa michezo ya kimataifa ya kuwania kombe la dunia. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
-
67
Jifunze Kiswahili: Maana na matumizi ya neno "MKWARUZO."
Katika kujifunza lugha ya Kiswahili hii leo Dkt. Mwanahija Ali Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anafafanua maana na matumizi ya neno "MKWARUZO."
-
66
09 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina. Kesho kutwa Alhamisi ya Juni 11, macho na masikio yanaelekezwa Mexico, Canada na hapa Marekani kwa ajili ya fainali za kombe la dunia kwa mpira wa miguu, au soka al maarufu kabumbu. Ingawa hivyo zama za sasa za mchezo huo maarufu zaidi duniani zinakumbwa na madhara ya athari za mabadiliko ya tabianchi. Ongezeko la joto kali linavuruga mechi na kuzua wasiwasi kuhusu mustakabali wa mchezo huo. Ni kwa kuzingatia hilo, Sekretarieti ya Mkataba wa Kimataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi, UNFCCC inamulika suala hilo na kutoa mapendekezo ya nini kifanyike kwani hivi sasa madhara ya joto kali kwenye kabumbu ni dhahiri. Feissal Kirwa anamulika hilo kupitia video iliyoandaliwa na UNFCCC.Pia tunakuletea muhtasari wa habari na jifunze Kiswahili.Takriban watoto milioni 138 duniani kote bado wako katika ajira za watoto, wakiwemo watoto milioni 54 wanaofanya kazi hatarishi. Hayo yamo katika ripoti mpya iliyotolewa leo na Shirika la Kazi la Umoja wa Mataifa ILO. Katika ujumbe wakwe kwenye ripoti hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa ILO, Gilbert F. Houngbo, ametoa wito wa kuchukuliwa hatua za haraka ili kubadili hali hii.“Habari njema ni kwamba hadi sasa tuna wagonjwa 19 ambao wamepona, hivyo utambuzi wa mapema na matibabu vinaokoa maisha,” Huyo ni Mkurugenzi wa Operesheni za Tahadhari na Hatua za Dharura za Afya wa Shirika la Afya la Umoja wa Mataifa Duniani (WHO), Dkt. Abdirahman Mahamud, akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva leo kwa njia ya video kutoka Bunia katika Jimbo la Ituri, nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC, jimbo ambalo linachangia asilimia 94 ya wagonjwa wote wa Ebola.Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu CRPD, umeanza leo Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York na utaendelea hadi 11 Juni. Kaulimbiu ya mwaka huu ni “kuadhimisha miaka 20 ya mkataba huo na kuimarisha utekelezaji wake katika dunia inayobadilika.” Washiriki wanajadili namna ya kutokomeza ukandamizaji, ukatili na manyanyaso dhidi ya watu wenye ulemavu, kuimarisha mifumo ya huduma na msaada, pamoja na kuongeza ushiriki na uwakilishi wao katika maisha ya kisiasa na umma.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anafafanua maana na matumizi ya neno "MKWARUZO."Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
-
65
Kevin Wekesa ambaye ni nyota wa raga anaongoza uchechemuzi wa mazingira kupitia michezo
Nyota wa mchezo wa raga ama rugby, Kevin Wekesa kutoka nchini Kenya ambaye alishiriki Michezo ya Olimpiki jijini Paris Ufaransa mwaka 2024, ameeleza nia yake ya kufanya vizuri uwanjani huku akitumia umaarufu wake kuhifadhi mazingira na kuhamasisha hatua endelevu kupitia michezo ili kujenga dunia yenye mnepo. Rashid Wekesa na taarifa zaidi.
-
64
08 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunaangazia ujumbe wa Katibu Mkuu kuhusu siku ya baharí duniani na kumulika ni hatua gani Zanziba zinachukua kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Pia tunakwenda nchini Kenya kufuatilia simulizi ya mchezaji wa raga.Bahari duniani zinakabiliwa na changamoto kubwa zinazotishia afya ya mazingira na ustawi wa binadamu, ameonya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres na kutoa wito wa hatua za haraka na za pamoja kukabiliana na hali hiyo.Jamii katika mkoa wa Kaskazini Unguja huko visiwani Zanzibar nchini Tanzania wanaadhimisha siku ya bahari hii leo Umoja wa Mataifa ukielezea dhahiri mafanikio ya mradi wa uhifadhi wa mikoko na ufugaji wa nyuki unaochagiza sio tu upatikanaji endelevu wa kipato bali pia uhifadhi wa mazingira na bahari.Nyota wa mchezo wa raga ama rugby, Kevin Wekesa kutoka nchini Kenya ambaye alishiriki Michezo ya Olimpiki jijini Paris Ufaransa mwaka 2024, ameeleza nia yake ya kufanya vizuri uwanjani huku akitumia umaarufu wake kuhifadhi mazingira na kuhamasisha hatua endelevu kupitia michezo ili kujenga dunia yenye mnepo.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
-
63
Mradi wa UNEP na wadau wake Zanzibar waimarisha uhifadhi wa bahari kupitia upandaji wa mikoko na ufugaji bora wa nyuki
Jamii katika mkoa wa Kaskazini Unguja huko visiwani Zanzibar nchini Tanzania wanaadhimisha siku ya bahari hii leo Umoja wa Mataifa ukielezea dhahiri mafanikio ya mradi wa uhifadhi wa mikoko na ufugaji wa nyuki unaochagiza sio tu upatikanaji endelevu wa kipato bali pia uhifadhi wa mazingira na bahari. Assumpta Massoi na maelezo zaidi ya mradi huo.
-
62
Lazima tujenge uhusiano mpya na bahari- Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa
Bahari duniani zinakabiliwa na changamoto kubwa zinazotishia afya ya mazingira na ustawi wa binadamu, ameonya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres na kutoa wito wa hatua za haraka na za pamoja kukabiliana na hali hiyo. Akizungumza kwa njia ya video katika ujumbe wake wa Siku ya Kimataifa ya Bahari inayoadhimishwa kila mwaka Juni 8, Bwana Guterres amesema bahari ni msingi wa maisha na maendeleo duniani, lakini zimekuwa zikikabiliwa na shinikizo linalozidi uwezo wake wa kustahimili."Bahari inaongoza tabianchi yetu, inalinda mifumo ya ikolojia na uchumi, na inalisha mabilioni ya watu duniani," anasema Guterres na kuongeza kuwa, "bahari ipo kwenye zahma kubwa na tunaishinikiza kupita uwezo wake."Guterres amerejelea Ripoti ya Tatu ya Tathmini ya Bahari Duniani iliyozinduliwa leo, ambayo imebainisha kuongezeka kwa athari za mabadiliko ya tabianchi, uvuvi uliokithiri, kupotea kwa bionuwai na uchafuzi wa bahari.Katibu Mkuu Guterres amesisitiza akisema, "hatuwezi kuendelea kuichukulia bahari kama kitu kisicho na ukomo," akihimiza kujengwa kwa uhusiano mpya na bahari unaozingatia sayansi, unaoongozwa na sheria za kimataifa na unaojengwa juu ya wajibu wa pamoja wa mataifa, sekta mbalimbali na vizazi vyote.Ametaja mafanikio ya Mkutano wa Tatu wa Bahari wa Umoja wa Mataifa uliofanyika mwaka jana pamoja na kuanza kutekelezwa kwa Makubaliano ya Baiyonuai ya Bahari katika maeneo yaliyo nje ya mamlaka ya kitaifa mwaka huu kama ushahidi kwamba ushirikiano wa kimataifa unaweza kuleta matokeo.Anasema, "hatua za pamoja za kimataifa zinawezekana na ni za lazima."Katika hitimisho la ujumbe wake wake, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amewataka viongozi wa dunia, sekta binafsi na wananchi kuchukua hatua kwa haraka ili kulinda bahari kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.Anasema, "katika Siku hii ya Kimataifa ya Bahari, hebu tuchukue hatua kwa nia thabiti na kutatua mahitaji ya wakati huu."Hakika yanayosemwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa yanaendana na aliyoyasema Mwenyekiti aliyechaguliwa wa ya Tume ya Kiserikali ya Bahari ya UNESCO (IOC) kwa Afrika na Nchi za Visiwa vinavyokaribia bara la Afrika (IOCAFRICA) Hellen Gichuhi alipozungumza na Idhaa ya Umoja wa Mataifa.
-
61
05 JUNI 2026
Jaridani tunakuletea mada kwa kina. Hii leo dunia inaadhimisha Siku ya Mazingira Duniani huku maadhimisho ya kimataifa yakifanyika jijini Baku nchini Azerbaijan. Maudhui ya mwaka huu ni "Sasa kwa ajili ya Tabianchi", yakiweka msisitizo mkubwa wa kuchukua hatua dhidi ya za uhifadhi wa mifumo ya ikolojia na hatua za kukabili tabianchi.Hivi karibuni, Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria pamoja na wadau, iliwasilisha Ripoti ya Hali ya Ziwa hilo ikionesha uwepo wa kemikali hatarishi, taka ngumu, plastiki, pamoja na majitaka vitu ambavyo ni hatari kwa viumbe wa majini na mazingira. Rashid Malekela wa Idhaa hii ametembelea mwalo wa Luchelele, uliopo mkoani Mwanza, kaskazini-magharibi mwa Tanzania, kufahamu jinsi wakazi wa eneo hilo wanavyochukua hatua dhidi ya Tabianchi. Anaanza na uongozi wa Kikundi cha Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi, BMU.Pia tunakuletea muhtasari wa habari zikiwemo za ... Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
-
60
Jifunze Kiswahili: Maana ya methali “La kiliwacho kisicholiwa ni sumu”
Katika kujifunza lugha ya Kiswahili, leo mchambuzi wetu ni Dkt. Josephat Gitonga, ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi nchini Kenya, kwenye kitivo cha Tafsiri na Ukalimani anafafanua maana ya methali “La kiliwacho kisicholiwa ni sumu”
-
59
04 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inatupeleka nchini nchini Rwanda. Kufuatia changamoto zinazoongezeka kutokana na mabadiliko ya tabianchi, kupanda kwa gharama za mbolea na ushindani wa masoko ya kikanda, Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo FAO linashirikiana na nchi ya Rwanda kutekeleza mkakati mpya wa kuimarisha sekta ya chai lengo likiwa ni kuboresha zao hilo na kuinua pato la mkulima.Mlinda amani wa Umoja wa Mataifa anayehudumu nchini Lebanon amefariki dunia na wengine wawili wamejeruhiwa mapema leo Alhamisi baada ya makombora ya mizinga kulenga eneo lao la kazi karibu na Marjayoun kusini mashariki mwa nchi hiyo, imesema taarifa ya Kikosi cha Mpito cha Umoja wa Mataifa nchini Lebanon UNIFIL. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anatarajiwa kutoa taarifa kuhusu tukio hilo muda wowote kuanzia sasa.Shirika la Umja wa Mataifa la afya Duniani, WHO, limesema chakula kisicho salama kinaendelea kuwa tishio kubwa kwa afya ya umma duniani, kikisababisha takribani wagonjwa milioni 866 na vifo milioni 1.5 kila mwaka, huku watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano wakiwa katika hatari kubwa zaidi. Kwa mujibu wa ripoti mpya watoto hao wadogo, ambao ni asilimia 9 tu ya idadi ya watu duniani, wanachangia karibu theluthi moja ya magonjwa yote yanayosababishwa na chakula.Leo ni siku ya watoto wasio na hatia waathirika wa ukatili duniani, maadhimisho haya yanakuja wakati ambapo ripoti ya Mwaka ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Watoto na Migogoro ya Silaha inaonesha kwamba ukatili dhidi ya watoto katika migogoro ya silaha ulifikia viwango visivyo vya kawaida mwaka 2024, huku kukiwa na ongezeko la asilimia 25 la ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu ikilinganishwa na mwaka uliopita.Na katika kujifunza lugha ya Kiswahili, leo mchambuzi wetu ni Dkt. Josephat Gitonga, ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi nchini Kenya, kwenye kitivo cha Tafsiri na Ukalimani anafafanua maana ya methali “La kiliwacho kisicholiwa ni sumu”."Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
-
58
Hifadhi ya Ngorongoro: Ambapo uhifadhi, utamaduni na utalii vinakutana kwa mustakabali endelevu
Tukilekea Siku ya Mazingira Duniani hapo Juni 5, Leo tunakupeleka katika moyo wa Tanzania Kaskazini mwa taifa hilo la Afrika Mashariki, ambako Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro inaendelea kuwa mfano wa jinsi binadamu, wanyamapori na urithi wa kitamaduni vinavyoweza kuishi pamoja huku vikichangia maendeleo ya utalii endelevu na ulinzi wa mazingira. Je nini kinafanyika kuhakikisha uhifadhi, utamaduni, mazingira na utalii vinakutana kwa mustakabali endelevu? Ili kupata majawabu Flora Nducha wa Idhaa hii amezungumza na Kamishna wa Hifadhi ya Ngorongoro, Abdul-Razaq Badru. Ungana nao
-
57
03 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inayotupeleka nchini Tanzania Kaskazini mwa taifa hilo la Afrika Mashariki, ambako Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro inaendelea kuwa mfano wa jinsi binadamu, wanyamapori na urithi wa kitamaduni vinavyoweza kuishi pamoja huku vikichangia maendeleo ya utalii endelevu na ulinzi wa mazingira. Je nini kinafanyika kuhakikisha uhifadhi, utamaduni, mazingira na utalii vinakutana kwa mustakabali endelevu? Ili kupata majawabu Flora Nducha wa Idhaa hii amezungumza na Kamishna wa Hifadhi ya Ngorongoro, Abdul-Razaq Badru.Mkurugenzi Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni WHO Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus ameendelea kusisitiza umuhimu wa ugunduzi wa mapema kwani hatua zikichukuliwa haraka wagonjwa wa Ebola wanapona. Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Geneva Usiswi baada kurejea kutoka ziarani mashariki mwa DRC amesema, Kufikia sasa, watu sita wamepona nchini DRC na wawili nchini Uganda, jambo linaloonesha kuwa watu wanaweza kupona Ebola iwapo watapata huduma za afya na kwenda vituo vya afya mara tu wanapoanza kuonyesha dalili za ugonjwa huo.Kuelekea kuanza kwa michuano ya Kombe la Dunia la FIFA wiki ijayo hapa Marekani na katika nchi jirani, Canada na Mexico, Shirika la Afya la Nchi za Amerika (PAHO) limetoa wito kwa nchi za bara la Amerika kuimarisha ufuatiliaji wa ugonjwa wa surua na Rubella kufuatia mikusanyiko mikubwa inayotarajiwa na milipuko inayoendelea ya surua na ongezeko la safari za kimataifa vinaweza kuongeza kasi ya kuenea kwa ugonjwa huo. Shirika hilo linazitaka mamlaka za afya kubaini maeneo yaliyo katika hatari kubwa na kuimarisha hatua za kukabiliana haraka ili kuzuia maambukizi zaidi. Na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa asubuhi hii kwa saa za New York, Marekani wanachagua wanachama watano wapya wasio wa kudumu wa Baraza la Usalama kwa muhula kipindi cha miaka miwili kuanzia tarehe 1 Januari 2027 hadi 31 Desemba 2028. Kutoka Barani Afrika mgombea mmoja ni Zimbabwe ambaye hata hivyo anatarajiwa kupita kwani hana mpinzani katika nafasi hiyo. Nchi zitakazochaguliwa zinachukua nafasi za Somalia, Pakistan, Panama, Denmark na Ugiriki, ambazo mihula yao itaisha mwishoni mwa mwaka huu 2026.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
-
56
Jifunze Kiswahili: Maana ya neno “CHOTORA”
Katika kujifunza lugha ya Kiswahili hii leo Mtalaam wetu Onni Sigalla kutoka Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania BAKITA anafafanua maana ya neno “CHOTORA”
-
55
02 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inayotupeleka nchini Jamhuri ya Kidokrasia ya Congo DRC katika mji wa Mavivi jimboni kivu kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo kusikia ni kwa jinsi gani walinda amani kutoka Tanzania wanaohudumu chini ya MONUSCO. wanavyochangia katika ulinzi wa amani na msaada wa kibinadamu.Umoja wa Mataifa umezitaka nchi zote duniani kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema baada ya kuthibitisha kuanza kwa hali ya El Niño, ukionya kuwa mabadiliko hayo ya joto la Bahari ya Pasifiki yataleta viwango vya juu vya joto kuliko kawaida karibu kila mahali duniani kati ya mwezi Juni mpaka Agosti na kuchochea matukio mabaya zaidi ya hali ya hewa. Akizungumza na waandishi wa habari jijini Geneva Uswisi Katibu Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Hali ya hewa duniani WMO, Celeste Saulo amesema "Taarifa hizi ni muhimu kwa sababu El Niño ni kichocheo kikubwa cha hali ya hewa duniani na mifumo ya mabadiliko ya tabianchi, bahari yenye joto, huongeza joto na unyevu kwenye mfumo wa hali ya hewa ambao unaweza kutumika kuzidisha hali mbaya ya hewa ikiwa ni pamoja na joto kali, na mvua kubwa.”.’Zinakaribia siku 100 sasa tangu kuanza kwa mzozo wa Mashariki ya Kati ambao athari zake zimesambaa duniani kote kwani umevuruga njia za usafirishaji na umeongeza gharama za usafiri na kuchelewesha utoaji wa huduma muhimu. Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya watoto UNICEF limeeleza kuwa fedha nyingi sasa zinatumika kwenye usafirishaji badala ya kununua vifaa vya kuokoa maisha ya watoto. Gharama za kusafirisha chanjo kwenda baadhi ya nchi barani Afrika zimeongezeka kwa hadi asilimia 70, huku gharama za kusafirisha chakula tiba, na vifaa vya elimu, nazo zikipanda kwa kiwango kikubwa. Shirika hilo linaonya kuwa hali hiyo inalazimisha kufanya maamuzi magumu kuhusu ni watoto gani wapate msaada kwanza". Mlipuko wa ugonjwa wa Ebola uliogundulika nchini Jamhuri ya Kidemokrasia Congo DRC na Uganda mwezi uliopita wa Mei ambapo mpaka sasa watu 49 wamepoteza maisha, 48 nchini DRC na mmoja nchini Uganda. Mkurugenzi Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni WHO Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus amezihimiza jumuiya za kimataifa kutoa usaidizi unaohitajika ili kudhibiti mlipuko. Pia amelihimiza nchi kutoweka vikwazo vya usafiri kwa DRC, ili kuhakikisha msaada wa kiafya na kibinadamu unaweza kufikia kiwango kinachohitajika.Na katika kujifunza lugha ya Kiswahili hii leo mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania, BAKITA. Anafafanua maana za neno "CHOTORA"Mwenyeji wako ni Rashid Malekela, karibu!
-
54
01 JUNI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina maalumu ambapo hii leo tutaelekea jijini Kampala nhcini Uganda kuangazia uzunduzi wa awamu ya tatu ya safari ya hija ya “Twende Zetu Butiama”, kumuenzi Hayati Mwalimu Julius Kmabarage Nyerere, rais wa zamani wa Tanzania aliyedumisha amani, msikamano na kupigania maendeleo ambazo ni ajenda zinazopewa kiaumbele cha juu na Umoja wa Mataifa. Shuhuda wetu katika uzinduzi huo uliofayika mwishoni mwa wiki alikuwa ni John Kibego kutoka Radio washirika wetu Kazi Njema FM ya mjini Hoima.Tukianza na ugonjwa wa Ebola lakini leo ni habari njema, wauguzi wanne waliokuwa wamelazwa hospitalini huko mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia Congo DRC wameruhusiwa kutoka hospitali baada ya kupona ugonjwa huo, na kufanya idadi ya waliopona virusi vya Ebola hadi sasa kufikia watu watano. Shirika la Umoja wa Mataifa la afya Duniani WHO katika taarifa yake limesema “Tunatarajia kuona watu zaidi wakipona, hasa wale wanaogunduliwa mapema na kupata huduma za afya kwa wakati, huku juhudi za kudhibiti mlipuko zikiongezwa kasi.”.’Kamati ya haki za watoto ya Umoja wa Mataifa imelaani sheria iliyopitishwa na uongozi wa Taliban nchini Afghanistan ya kuwa mtoto wa kike akisha balehe tu tayari anaweza kuolewa. Kamati imesema sheria hiyo mpya ni ukiukwaji mkubwa na wakimfumo wa sheria ya kimataifa ya haki za binadamu na kwamba Taliban wanachukulia ukimya wa wasichana kama ridhaa, na kwamba amri hiyo ni muendelezo wa mfululizo wa hatua za kibaguzi zinazochukuliwa na utawala wa Taliban,".Na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, hii leo ameonya kuwa kuenea na kuhamishwa kwa njia haramu kwa silaha ndogo ndogo na nyepesi kunaendelea kuchochea migogoro, ugaidi, uhalifu na ukatili wa kijinsia duniani kote, huku akizitaka nchi kuimarisha ushirikiano wa kimataifa ili kukabiliana na vitisho vinavyoibuka.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
-
53
29 MEI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina maalumu ambapo tunamwangazia mmoja wa maafisa waandamizi wa Umoja wa Mataifa, Joyce Msuya. Mwisho wa wiki hii, Joyce, raia wa Tanzania ambaye pia amewahi kuhudumu katika Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo, UNEP na pia Benki ya Dunia anahitimisha utumishi wake katika Umoja wa Mataifa akiwa Msaidizi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya kibinadamu na pia Naibu wa Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Misaada ya Kibinadamu (OCHA). Katika mazungumzo haya na Anold Kayanda wa Idhaa hii, Joyce Msuya anaanza kwa kuitafari miaka minne aliyohudumu katika nafasi hii.Jamhuri ya Kidemokrasia Congo DRC inakumbwa na ugonjwa wa Ebola ambapo Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya duniani WHO, Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus amefika huko na anaeleza sababu. ‘Nimefika hapa kuzieleza jamii za Ituri, Kivu Kaskazini na Kivu kusini kuwa hawako pekeyao, na kwamba tupo hapa kuwaunga mkono, na tunaelewa machungu yao, lakini pia tunafahamu wana nguvu na yote yanayohitajika kukomesha hili. Ninatumia fursa hii kuziomba jumuiya za kimataifa kuongeza usaidizi wao ili wahudumu wa afya waweze kupata vifaa tiba na vya kujilinda na maambukizi.’Kupigwa marufuku watoto kutumia mitandao ya kijamii, si suluhisho la mara moja kwa suala mtambuka lenye sura nyingi, ndio maana hii leo Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk ametaka hatua kali zichukuliwe na kila nchi, pamoja na makampuni ya teknolojia, ili kufanya mitandao ya kijamii kuwa salama zaidi kwa watoto, akisisitiza udhibiti, usimamizi na uwajibikaji unaofaa. Kamishna Türk amesema "Kuimarisha ulinzi wa watoto mtandaoni ni kipaumbele cha dharura ambacho tunahitaji kuhakikisha sio tu kwamba kinafanyika, bali pia kinafanyika ipasavyo,".Na ukatili wa kingono kwenye maeneo yenye migogoro ulifurutu ada mwaka 2025, hii inamanisha kuna ongezeko kubwa la ukatili wa kingono huku wanawake na wasichana ndio idadi kubwa ya waliokumbwa na madhila hayo yaliyohusisha pia waathirika hao kuuawa baada ya kubakwa. Haya yamebainika kwenye ripoti ya ukatili wa kijinsia unaohusiana na migogoro iliyotolewa na Umoja wa Mataifa leo ambayo pia imeonya kuwa kuongezeka kwa matumizi ya kijeshi duniani na kupungua kwa bajeti za misaada ya kibinadamu kulidhoofisha uwezo wa serikali na taasisi kuzuia na kuchunguza ukatili huo wa kingono. Ripoti hiyo imetoa wito wa kuchukuliwa hatua madhubuti zaidi za kimataifa pamoja na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa fedha ili kulinda raia, na kuwasaidia manusura wa ukatili wa kingono unaohusiana na migogoro.Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
-
52
28 MEI 2026
Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inayomulika nchi zinazochangia vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Mataifa, ikiwa ni pamoja na Taifa la Tanzania na Balozi Togolani Idriss Mavura mara baada ya kuwasilisha hati zake za utambulisho kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amezungumza na Flora Nducha kuhusu suala hili muhimu.“Nataka niwe mkweli; hii ni moja ya changamoto zetu kubwa zaidi. Hatuwezi kufanya kazi hii kama wale wanaojaribu kusaidia wanazuiwa kufanya hivyo, au kuwekwa katika hatari.” Ni sehemu ya barua ya Dkt. Tedros Ghebreyesus, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni, WHO, aliyowaandikia wananchi wa Jamhuri ya Kidemorkasia ya Congo, DRC wakati huu vikwazo kama vile mapigano jimboni Ituri, yanakwamisha harakati za kudhibiti mlipuko wa 17 wa Ebola nchini humo.Vikwazo vingine vya kudhibiti Ebola nchini DRC ni mila. Maki Baraka mkazi wa Beni jimboni Kivu Kaskazini ambako Ebola imeripotiwa mji jirani wa Butembo ana wito.Na Joyce Msuya, Naibu Mkuu wa Ofisi ya UN inayoratibu misaada ya dharura, OCHA anatamatisha jukumu lake baada ya kuhudumu kwa miaka minne. Anold Kayanda amemuuliza anachokumbuka zaidi.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
-
51
Jifunze Kiswahili: Maana na matumizi ya neno "PEKEPEKE."
Katika kujifunza lugha ya Kiswahili, hii leo Dkt. Mwanahija Ali Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anafafanua maana na matumizi ya neno "PEKEPEKE."
We're indexing this podcast's transcripts for the first time — this can take a minute or two. We'll show results as soon as they're ready.
No matches for "" in this podcast's transcripts.
No topics indexed yet for this podcast.
Loading reviews...
Loading similar podcasts...